Saturday 5 April 2014

Yala: Shule iliyogeuka ‘kisiwa’


 Sehemu ya Shule ya msingi Yala ikiwa  imejaa maji. 


Yala ni shule ya msingi iliyopo katika Kijiji cha Yala Kata ya Luhanga Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya na ipo umbali wa kilomita 40 kutoka Barabara Kuu ya Mbeya-Iringa, ili kufika shuleni hapo inakulazimu kutembea kwa mguu kutokana na magari na pikipiki kushindwa kufika.

Shule hiyo ina muda wa zaidi ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwake, imezungukwa na mito minne ambayo imekuwa ikijaa maji kipindi cha masika na kusababisha kukatika kwa mawasiliano na ukosefu wa huduma mbalimbali ikiwa ni pamoja na elimu.
Kutokana na tatizo hilo la mito kujaa maji shule hiyo imekuwa ikigeuka kuwa kisiwa na kusababisha wanafunzi na walimu kushindwa kufika shuleni kwani mito hiyo haina madaraja ya kuwawezesha kupita na kufika shuleni hapo.
Wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo wamekuwa wakitoka katika Vitongoji vya Mwashikamile, Ruaha, Waninyika, Mtakuja, Yala na Lusaka na wote hushindwa kuvuka mito hiyo na kufika shuleni huku walimu pia wakikumbwa na adha hiyo kutokana na shule hiyo kutokuwa na nyumba za kuishi Walimu.
Jairos Mpale ni Mwenyekiti wa serikali ndogo ya maendeleo ya Mwashikamile katika Kijiji cha Yala anasema kuwa tatizo hilo limekuwa kubwa zaidi kwa mwaka huu ukilinganisha na miaka mingine.Hii ni kutokana na mvua zinanyesha kwa wingi na wanafunzi wamekaa nyumbani muda mrefu bila kwenda shule.
“Watoto wetu wameshindwa kwenda shuleni hapo tangu shule zote zilipofunguliwa Januari, kutokana na mito kujaa maji na kuna mamba wengi na viboko hivyo ni vigumu kuvuka kwenda katika Shule ya Yala na watoto wetu wamekosa masomo na hatujui ni lini wataanza masomo,” anasema.
Naye Mtendaji wa kijiji cha Yala shule ilipo, Isaac Ngera anasema kuwa tatizo hilo huwa linajitokeza mara kwa mara katika msimu wa mvua na mito hiyo imekuwa ikijaa na kusababisha wananchi kushindwa kupata huduma mbalimbali za kijamii ikiwa ni pamoja elimu, afya na majisafi na salama.
Aliitaja mito iliyojaa maji kuwa ni Itambo na lwashimala na vitongoji vilivyopo ng`ambo ya mito hiyo ni Ruaha na Woninyika kwa upande wa Kusini kuna vitongoji vya Mtakuja na Lusaka ambavyo vipo ng`ambo ya Mto Itambo na yote imejaa maji hakuna mawasiliano na upande wa pili.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Stephano Mlewa anasema kuwa kwa sasa hali ni mbaya katika shule hiyo kwani hakuna mwanafunzi anayefika shuleni hapo.
“Siyo kwa wanafunzi pekee hata kwa Walimu ni tatizo kubwa kwani wanaishi katika kitongoji ambacho kipo mbali na shule hiyo na inawalazimu wavuke mito miwili ambayo kwa sasa imejaa maji hivyo hakuna masomo,” anasema.
Anasema kuwa shule hiyo pia ina changamoto ya madarasa kwani ina jumla ya vyumba vya madarasa vinne pekee na wanafunzi wapo kuanzia darasa la kwanza hadi la saba hivyo husoma kwa kupokezana.
Ofisa Elimu Wilaya ya Mbarali, Henerico Batinoluho anasema kuwa shule ina wanafunzi zaidi ya 400 na kwamba mwaka huu shule ilifunguliwa Januari 6, lakini wamefanikiwa kuingia darasani katika kipindi cha wiki moja pekee.

No comments:

Post a Comment