Saturday 12 July 2014

KWA WALE WALIO MBAL NA WAPENZ MAWASILIANO NI MUHIMU

Wewe ni mwanamke au mwanaume ulikuwa na mpenz wako Yawezekana mlikuwa mnafanya kazi pamoja lakini mmoja akahamishiwa mkoa mwingine au mlikuwa mnasoma pamoja na kuanzisha uhusiano lakini baada ya kumaliza masomo kila mmoja akarudi kwao na kujikuta mkiwa mbali mbali licha ya kwamba mnapendana kwa dhati.

Katika mazingira hayo, bado uhusiano wenu unaweza ukaendelea na kila mmoja akajisikia amani moyoni mwake, kwa vipi? Kwa kuzingatia haya ambayo nitayaeleza katika mada yangu ya leo yanayokitia chumvi kichwa cha habari hapo juu kinachosema, wa kuliua ama kulidumisha penzi na mpenzi wako aliye mbali ni wewe!

Funga safari, mtembelee

Kufanya safari ya mshtukizo ni kati ya mambo ambayo yatamfanya mwenzi wako afurahi. Lakini lazima uwe makini kabla ya kufanya jambo hili. Ni vyema ukawa na uhakika kwamba mna kipindi kirefu hamjakutana na kila mmoja (hasa yeye) ana shauku sana na wewe.

Nenda bila kumtaarifu, fikia hotelini, kisha mpigie simu ukijifanya upo sehemu ambayo alikuacha. Baada ya hapo, ukishahakikisha umeteka hisia zake sawia, sasa unaweza kumweleza ukweli kwamba upo katika makazi yake mapya.

Hakika itakuwa furaha kubwa, ingawa pia inawezekana ikawa huzuni, hasa kama alikuwa anakusaliti. Kama ikiwa hivyo, si haba kwani angalau utakuwa umefahamu ukweli kwamba mwenzi wako hakuwa wako, kwani ni msaliti na aliyekuwa anakupotezea muda wako. Sina shaka utakuwa mpya!


Mawasiliano ya mara kwa mara
Kuwasiliana na mpenzi wako mara kwa mara, kunatajwa kama njia mojawapo kati ya nyingi zinazoweza kukusogeza karibu zaidi na mpenzi wako aliye mbali na hivyo kulitia mbolea penzi lenu.


Hata hivyo, wengi hushindwa kujua aina ya mawasiliano na jinsi ya kutumia ili kuteka akili za wapenzi wao na kuwafanya waendelee nao siku zote licha ya kuwa mbali nao.


Kutokana na hilo nimeamua kuwaletea dondoo za mawasiliano ambazo zinaweza kutumika katika kumvuta mpenzi wako.

Kumwandikia email au kwa kiswahili tunaita baruapepe. Njia hii ya mawasiliano kwa wapenzi walio mbali ni nzuri sana. Hata hivyo, inategemea mpenzi wako yuko wapi, maana kuna maeneo mengine hayana huduma za Mtandao wa Internet.


Kutokana na kukua kwa Teknolojia, wengi humiliki kompyuta za mikononi (lap top) ambazo huwarahisishia mawasiliano ya moja kwa moja na watu wengi. Kama mpenzi wako ni mmoja wao, hii ni nafasi nzuri sana kwako.


Mtumie kadi nzuri zenye ujumbe mwanana wa mapenzi kwa ajili ya kuhamasisha penzi, mwandikie tungo za mapenzi ukionyesha ubunifu wako. Pia waweza kumtumia vichekesho kwa ajili ya kumburudisha na kumfanya mwenye furaha.

Kumpigia simu au kumtumia sms. Kuwasiliana kwa njia ya simu za mkononi ni moja kati ya njia bora za mawasiliano na kuboresha uhusiano wa wapenzi. Mwenzi wako anapokuwa mbali na wewe, kwa kutumia njia hii, unaweza kumsogeza karibu yako na kufurahia uwepo wako, ingawa yupo mbali na wewe.


Umpigiapo simu lazima maneno yako yawe laini, zungumza naye kwa unyenyekevu na kumtia hamasa ya kuzidi kuzungumza na wewe. Kadhalika unapomwandikia meseji, kaa chini na utunge, siyo unamwandikia ‘sema mtu wangu, uko shwari? Umeshakula?’. Hii si meseji ya kumtumia mpenzi wako aliye mbali na wewe.

Unapaswa kumtumia sms za mapenzi, tungo za mahaba, maneno ya utani, vichekesho na kejeli ni kati ya vitu vya kufurahisha ambavyo vikifanywa, humfanya mwenzi wako kutokuwa tayari kukusaliti.

Unaweza kumtumia meseji nyingi kadri uwezavyo kulingana na uwezo wako wa fedha, ingawa mitandao mingi ya simu za mkononi siku hizi huwa na ofa maalum ya kutuma sms nyingi kwa gharama ndogo! Unaweza kujisajili kila siku kwa ajili ya kurahisisha mawasiliano na mpenzi wako.

Pamoja na kwamba uwezo wako kifedha, muda na majukumu vinaweza kukufanya uamue idadi ya sms utakazomtumia mpenzi wako, lakini ni lazima umtumie angalau sms tano kwa siku.
Meseji hizo hutumwa kwa muda maalum kama vile baada ya kuamka asubuhi ambapo unapaswa kumtumia ujumbe mzuri wa kumtakia asubuhi njema na mafanikio katika kazi zake za kutwa hiyo.


Mchana, mtakie mlo mwema na kazi njema, alasiri mtumie ujumbe wa kichekesho. Usiku, mtumie ujumbe wa kumpa pole kwa kazi, kisha malizia kwa kumtumia ujumbe mwanana wakati wa kulala. Kama nilivyoeleza awali, unaweza kutuma meseji nyingi zaidi kulingana na uwezo wako na muda huku ukizingatia majukumu yako ya kazi.

No comments:

Post a Comment