Thursday 16 May 2013

UNAJUA VYAKULA AMBAVYO NI HATARI KWA AFYA YAKO?NA UNAPASWA UVIOGOPE?soma hapa......


Kila siku tupo katika kujifunza. Hakuna mwanadamu yeyote aliyezaliwa akiwa anajua kila kitu. Kujifunza ni wajibu wa kila binadamu na hasa kujifunza mambo muhimu yanayohusu maisha yetu ya kila siku.

Katika kujifunza masuala ya vyakula bora na visivyo bora, katika makala yetu ya leo tunajifunza baadhi ya vyakula ambavyo si salama kwa afya zetu, hata kama tumekuwa tukidhani hivyo kwa miaka yote iliyopita.

Baadhi ya vyakula vifuatavyo, vimethibitika kuwa na madhara katika afya ya binadamu na tumeshauriwa kuviepuka. Ingawa ni vyakula tunavyovitumia kila siku, lakini inatupasa sasa kukubali tulikuwa hatujui na sasa tumejua, hivyo tuviepuke:

NYANYA YA KOPO (Canned Tomatoes)
Kwa mujibu wa mtaalamu Fredrick vom Saal (PhD) wa Chuo Kikuu cha Missouri nchini Marekani, utengenezaji wa kopo la kuhifadhia nyanya kwa ndani, hutumia kemikali aina ya ‘bisphenol-A’ ambayo inaaminika kuwa chanzo cha matatizo ya uzazi, magonjwa ya moyo, kisukari na unene pamoja na gesi tumboni (acidity).

Mbali na kopo lenyewe kutokuwa salama, ili kuihifadhi nyanya isiharibike haraka, lazima iongozewe vitu (additives) na kuwekewa kemikali za kuhifadhia chakula (preservatives) ambavyo navyo kwa ujumla wake siyo salama kiafya. Kwa msingi huo, huna sababu ya kutumia nyanya za kopo wakati nyanya halisi zipo tele sokoni.
NYAMA YA NG’OMBE WANAOLISHWA MAHINDI (Corn- Fed Beef).

Kwa mujibu wa mtaalamu Joel Salatin kutoka Kampuni ya Polyface Farms na mwandishi mashuhuri wa vitabu kuhusu kilimo bora chini Marekani, ng’ombe kwa kawaida ameumbwa kuishi kwa kula majani, siyo nafaka.

Lakini sasa wafugaji huilisha mifugo yao nafaka, ikiwemo soya na kufanya mifugo kunenepeana kuliko kawaida, kwa lengo la kuchinja ng’ombe walionona ili kujipatia faida zaidi. Nyama itokanayo na mfugo wa aina hiyo inakosa uhalisia wake na hivyo kuwa na madhara kwa mlaji.

Katika utafiti mmoja uliofanywa hivi karibuni, imebainika kuwa ukilinganisha na ng’ombe wanaolishwa nafaka, wale wanaolishwa majani, nyama zao zina kiwango kingi cha virutubisho kama vile Carotene, Vitamin E, Omega 3, Calcium, Magnesium na Potassium.

VIAZI VYA KUOTESHWA KWA MBOLEA (Non Organic Potatoes)
Kwa mujibu wa mtaalamu Jeffrey Moyer, Mwenyekiti wa Bodi ya masuala ya vyakula asilia, vyakula vyote vitokanavyo na mizizi (viazi, mihogo, n.k) havitakiwi kuoteshwa kwa mbolea wala kumwagiliwa dawa za kuulia wadudu (pesticides), kwa sababu vina kawaida ya kunyoya ardhini kemekali hizo.

Ulimaji wa kisasa kwa baadhi ya wakulima, hasa katika nchi zilizoendelea, viazi huoteshwa kwa kutumia mbolea, humwagiliwa dawa za kuulia wadudu na hata wakati wa kuchimba na kuvuna, bado viazi hivyo huwekewa tena dawa za kuzuia visiote au kuharibika. Ulimaji huu hukifanya kiazi au muhogo kuwa sumu.

Hivyo basi, inashauriwa tulime viazi na mihogo kwenye udongo wenye rutuba ya asili au kwa kutumia mbolea asilia, kama vile majani au kinyesi cha ng’ombe na tuepuke kutumia mbolea nyingine zenye kemikali au sumu. Kwa kufanya hivyo tutakula viazi na mihogo na kupata faida ya vyakula hivyo asilia.

MAZIWA YA NG’OMBE WALIOLISHWA DAWA (Milk Produced with artificial hormones)
 Mtaalamu Rick North anayejishughulisha na masuala ya vyakula salama anasema kuwa baadhi ya wafugaji wa ng’ombe wa maziwa huwalisha ng’ombe wao vichocheo bandia vya mwili (artificial hormones) vya kuzalisha maziwa (rBGH or rBST) ili kuifanya mifugo yao izalishe maziwa mengi.

Kitendo hicho, hufanya maziwa yatokanayo na ng’ombe aliyelishwa vichecheo hivyo kutokuwa salama na inaelezwa kuwa maziwa ya aina hiyo pia yameonekana kusababisha saratani za matiti, kibofu cha mkojo na tumbo kwa mnywaji.

Hivyo chonde chonde wafugaji wa mijini, walisheni ng’ombe wenu wa maziwa vyakula vya asili walivyoumbiwa na Mungu, ambavyo ni majani na siyo madawa kwa sababu ni hatari kwa afya ya mlaji.

No comments:

Post a Comment