Thursday 27 February 2014

Uamuzi wa Museveni waitia kiwewe Marekani


Rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni akitia saini muswada wa sheria dhidi ya wapenzi wa jinsi moja kwenye Ikulu ya Entebbe juzi. Muswada huo sasa unakuwa sheria kwa ajili ya kutumika kuwashughulikia watu wenye hulka hiyo. Picha na Daily Monitor.  
 

Kampala. Siku moja baada ya Rais Yoweri Museveni kusaini sheria inayotoa adhabu kali kwa wapenzi wa jinsi moja, Marekani imesema inaangalia upya uhusiano wake na nchi hiyo kama ilivyoainisha awali.
Katika taarifa yake iliyotolewa jijini Washington DC jana, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry alisema Serikali ya Rais Barack Obama itahakikisha ushirikiano wowote na Uganda utachujwa kupitia sheria za kupinga ubaguzi ambazo inazisimamia.
“Sheria imeshapitishwa, tunaanza kuchuja uhusiano wetu na Uganda kwa kuangalia mambo muhimu, ikiwemo maeneo tunayowawezesha,” alisema Kerry katika taarifa yake jana.
Awali, akitia saini muswada huo kuwa sheria juzi, Rais Museveni alipuuza vitisho vya Marekani na kusema mataifa ya nje ambayo yamekuwa yakimtaka asisaini muswada huo pamoja na viongozi wa kidini hawana nafasi katika mambo ya ndani ya nchi yake.
“Watu  kutoka nje hawawezi kutuamuru tufanye au tusifanye mambo yetu. Kama hawataki kwenda nasi, basi wanaweza kuchukua misaada yao,” alisema.
Akizungumzia onyo lililotolewa na baadhi ya viongozi wa kidini akiwemo Askofu Desmond Tutu wa Afrika Kusini, Museveni alisema: “Kumbuka hata Yesu aliuawa na maaskofu, ndiyo maana huwa sisikilizi watu hao (viongozi wa kidini).”
Mataifa ya Afrika yenye sheria kama iliyopitishwa Uganda
Wakati Marekani na baadhi ya washirika wao wakitishia kuzuia misaada kwa Uganda, mataifa mengi ya Afrika, isipokuwa Afrika Kusini yana sheria kali za kupiga marufuku wapenzi wa jinsi moja. Sheria zimekuwa zikitekelezwa kwa muda mrefu sasa.
Shirika la Haki za Binadamu, Amnesty International linasema uhusiano wa kimapenzi wa watu wa jinsi moja umeharamishwa kisheria katika nchi 38 kati ya 54  barani humo  na adhabu ya kifo imehalalishwa nchini Mauritania, Sudan na Somalia.
Nchi zilizoweka sheria kali kuwabana wapenzi wa jinsi moja ni pamoja na Uganda ambayo imepiga marufuku wapenzi wa jinsi moja na  kutoa adhabu ya hadi kifungo cha maisha gerezani kwa wale wanaorudia vitendo hivyo.
Sheria hiyo inazuia kutangaza masuala yahusuyo wapenzi wa jinsi moja na kuwataka watu kuwatenga na kuwakataa mashoga.
Nigeria,  pia imeweka sheria maalumu iliyoanza kutekelezwa Januari mwaka huu. Sheria hiyo inatoa adhabu ya kifungo cha hadi miaka 14 jela kwa wapenzi wa jinsi moja wanaoishi pamoja.

No comments:

Post a Comment