Arusha.
  Mamia ya wafuasi
 wa Chadema jana, waliandamana katikati ya jiji, wakati mvua ikinyesha 
wakimtembeza Diwani mpya wa Kata ya Sombetini, Ally Benanga huku, 
viongozi wakitoa kauli kuwa siku za Meya wa Jiji la Arusha, Gaudence 
Lymo kukaa madarakani zinahesabika.
Mamia ya wafuasi hao, wakiongozwa na mbunge wa 
Jimbo la Arusha, Godbless Lema,aliyekuwa kwenye gari la wazi la Benanga,
 bila kujali mvua waliandamana kutoka ofisi za chama hicho hadi Jiji la 
Arusha kwa kupita barabara za Sokoine na baadaye kurejea katika ofisi za
 chama hicho, eneo la Ngarenaro.
                
              
Hata hivyo, ingawa maandamano hayo, yalikuwa 
hayana kibali, polisi walilazimika kuyasindikiza ili kuepusha vurugu 
kubwa na hakuna vurugu ambayo ilitokea.
                
              
Watangaza kumng’oa Meya
                
              
Akizungumza mara baada ya maandamano hayo, 
Mwenyekiti wa Vijana wa Chadema Mkoa wa Arusha,, Ephata Nanyaro, ambaye 
pia ni Diwani wa Kata ya Levolosi, alisema baada ya kupata ushindi wa 
Kata ya Sombetini, kazi ambayo ipo mbele yao ni kumng’oa Meya kwani wana
 idadi ya kutosha kuongoza jiji kwa sasa.
                
              
“Tayari tumeandaa tuhuma zake na tutapeleka jiji 
kuomba kikao maalum cha Baraza la Madiwani ambacho kitakuwa na ajenda 
moja tu juu ya utendaji wa Meya”alisema Nanyaro.
                
              
Alisema kikao hicho, kitakuwa cha wazi na akaomba 
wakazi wa jiji, kujitokeza wakipata taarifa kwani, tuhuma ambazo 
watatumia kumng’oa Meya Lymo zipo wazi .
                
              
Naye Lema akizungumza na mamia ya wakazi wa Jiji 
la Arusha, aliwapongeza kwa kumchagua diwani wa Chadema Kata ya Sombetni
 na sasa kufanya Chadema kuwa na jumla ya madiwani pamoja na wabunge 16 
katika jiji la Arusha..
                
              
“Kuanzia sasa sisi ndiyo tutaongoza Jiji, 
tunawahakikishia tutashughulikia matatizo yenu ya ukosefu wa huduma bora
 za afya, barabara, viwanja, elimu na nyingine i”alisema Lema.
                
              
Alisema hivi sasa Jiji lina mpango wa kugawa 
viwanja na watakaonufaika ni watu kawaida walio na shida ya ardhi na 
siyo viongozi kama ambavyo imezoeleka kwa kuwa kamati ya mipango miji 
sasa itakuwa chini ya uongozi na usimamizi wa Chadema.
                
              
    
    
     
 
 
No comments:
Post a Comment