
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industries Limited (TPI), Ramadhani Madabida (kulia) na Ofisa Ubora wa Bidhaa wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD), Evance Mwemezi walipofikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam jana kusomewa mashtaka ya kuuza na kusambaza dawa feki za ARV.
Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Ltd cha Dar es Salaam (TPI), Ramadhani Madabida na wenzake watano wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka matano likiwamo la kusambaza dawa bandia na kusababisha hasara ya Sh148.3 milioni.
Wakili wa Serikali, Faraja Nchimbi aliwataja 
washtakiwa wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo kuwa ni Mkurugenzi wa 
Operesheni wa TPI, Seif Shamte, Meneja Masoko, Simon Msofe, Mhasibu 
Msaidizi, Fatma Shango pamoja na wafanyakazi wa Bohari ya Dawa (MSD), 
Sadick Materu na Evans Mwemezi.
                
              
Akisoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi wa 
Mahakama hiyo, Nyigulile Mwaseba, Wakili wa Serikali, Shadrack Kimaro 
alisema katika shtaka la kwanza, Aprili 5, 2011, Madabida, Shamte, Msofe
 na Shango wakiwa na nyadhifa hizo kwenye kiwanda cha TPI walisambaza 
makopo 7,776 ya dawa bandia za kufubaza virusi vya Ukimwi (ARV) aina ya 
Antirectroviral.
                
              
Kimaro alidai kuwa washtakiwa hao, walifanya kosa 
hilo kinyume na kifungu cha 76 (1)(2) cha Sheria ya Chakula, Dawa na 
Vipodozi ya mwaka 2003, wakijaribu kuonyesha kuwa dawa hizo zilikuwa 
halali na kwamba zimetengenezwa Machi, 2011 na muda wake wa kutumika 
unakwisha 2013 wakati wakijua kuwa si kweli.
                
              
Katika shtaka la pili, Wakili Kimaro alidai kuwa 
Aprili 11, 2011, Madabida, Shamte, Msofe na Shango walisambaza na kuuza 
makopo 4,476 ya dawa bandia aina ya Antiretroviral walizokuwa wakijaribu
 kuonyesha kuwa zilikuwa na viambatanisho vya Starudine 30mg, Nevirapine
 200mg, Lamivudine 150mg pamoja na fungu namba OC 01.85.
                
              
Alidai kuwa washtakiwa hao waliweka viambatanisho 
hivyo wakijaribu kuonyesha kuwa dawa hizo zilikuwa halisi na kwamba 
zilitengenezwa Machi 2011 na muda wake wa kutumika ulikwisha Februari 
2013 huku wakijua kwamba ni uongo.
                
              
Katika shtaka la tatu wanadaiwa kujipatia fedha 
kwa njia ya udanganyifu, kinyume na Kifungu cha 302 cha Sheria ya Kanuni
 ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
                
              
Wakili Kimaro alidai kuwa kati ya Aprili 12 na 29,
 2011, washtakiwa hao wakiwa na nia ya kulaghai, walijipatia Dola za 
Marekani 98,506 sawa na Sh148,350,156.48 wakijaribu kuonyesha kuwa kiasi
 hicho cha fedha ni malipo halali ya makopo 12,252 ya dawa aina ya 
Antirectrovial yaliyokuwa katika fungu (batch) namba OC 1.85.
                
              
Alidai pia kuwa washtakiwa hao walikuwa 
wakionyesha dawa hizo bandia zilikuwa zimetengenezwa Machi, 2011 na 
kwamba muda wake wa kumalizika kutumika ni Februari, 2013 na 
wakafanikiwa kujipatia kiasi hicho cha fedha kutoka MSD.
                
              
Katika shtaka la nne, Materu na Mwemezi wakiwa ni 
Meneja wa Udhibiti Viwango na Ofisa Udhibiti Viwango wa MSD, kati ya 
Aprili 2 na 13, 2011 huku wakijua nia ya kutendeka kwa makosa hayo ya 
usambazwaji wa dawa bandia, walishindwa kuzuia kinyume na Kifungu cha 
Sheria namba 383 cha Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa 
marekebisho mwaka 2002.
                
              
Katika shtaka la tano, wakili huyo wa Serikali 
alidai kuwa kati ya Aprili 5 na 30, 2011, washtakiwa Madabida, Shamte, 
Msofe, Shango pamoja na Materu na Mwemezi, kinyume na Sheria ya Uhujumu 
Uchumi, walishindwa kutekeleza majukumu yao wakiwa watendaji.
                
              
Alidai kuwa katika kipindi hicho, washtakiwa hao 
kwa pamoja walishindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kusambaza 
makopo 12,252 ya dawa bandia wakijaribu kuonyesha kuwa zilitengenezwa 
Machi 2011 na kwamba zitakwisha muda wake wa kutumika Februari 2013 na 
kuisababishia mamlaka hiyo ya Serikali hasara ya Sh148,350,156.48.
Washtakiwa wote walikana mashtaka yanayowakabili na upande wa 
mashtaka ulisema upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika. Akitoa 
masharti ya dhamana, Hakimu Mwaseba alimtaka kila mshtakiwa kuwa na 
wadhamini wawili wanaoaminika ambao wanafanya kazi kwenye taasisi 
zinazotambulika kisheria na kwamba kila mdhamini angesaini bondi ya 
Sh6,181, 256.
                
              
Pia alimtaka kila mshtakiwa kutoa kiasi cha Sh12, 
362,513 milioni taslimu mahakamani hapo au hati ya mali isiyohamishika 
yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.
                
              
Madabida na Materu waliachiwa huru baada ya kukamilisha masharti hayo huku wenzao wakipelekwa mahabusu kusubiri kuyakamilisha.
                
              
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 24, mwaka huu itakapotajwa.
 
 
 
No comments:
Post a Comment