Monday 17 February 2014

Vyakula vya watoto vyadaiwa kuwekwa dawa za kulevya

Ni mbinu ya wauzaji kuongeza idadi ya watumiaji,inasemekana huwekwa kwenye vyakula vya watoto.


Dar es Salaam. Tahadhari imetolewa kwa wazazi kuwa makini na vyakula wanavyokula watoto wao kufuatia kuibuka kwa mbinu mpya ya wauzaji dawa za kulevya kuweka dawa zao hizo kwenye vyakula vinavyopendwa na watoto.
Akihutubia kwenye mkutano wa Baraza la Vijana wa Wilaya ya Temeke, Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile amesema, wauzaji wa dawa za kulevya kila siku wamekuwa wakibuni njia mpya za kuhakikisha wanapata kundi kubwa la watumiaji wa dawa hizo.
Katika kuhakikisha dhamira yao hiyo inatimia, hivi sasa wamebuni njia mpya ya kuweka dawa hizo kwenye vyakula vidogo vidogo vinavyopendwa na watoto kama vile kashata na ubuyu.
“Ni jukumu letu sote pamoja na nyinyi vijana ni kuelekeza nguvu zetu katika mapambano ya dawa za kulevya kwani, kwa sasa yanaonekana kuwa janga la kitaifa kutokana na kuathiri nguvu kazi kubwa ya taifa letu,” alisema.
Amesema takwimu za kitaifa za matumizi ya dawa za kulevya kwa Wilaya ya Temeke siyo nzuri kwani zinasikitisha mno, kwani mmoja kati ya wanawake watatu wanaotumia dawa hizo ameathirika na Ukimwi huku wa wanaume wawili kati ya wanne wameathirika na Ukimwi.
Kuhusu magonjwa mengine, amesema kama yale ya homa ya ini pia ni hatari kwa afya na huwaandama vijana hao.
Naye Mwenyekiti wa Vijana wa Wilaya ya Temeke, Oliver Mwambope amesema, kutokana na ukweli kuwa vijana hujiingiza kwenye wimbi la matumizi ya dawa za kulevya, chama chake kimeweka utaratibu maalumu wa kupambana na tabia zote hatarishi zikiwamo zile za matumizi ya dawa hizo.
Mara kwa mara tumekuwa tukiendesha kampeni za kupambana dawa za kulevya pamoja na tabia nyingine hatarishi.
Pamoja na utaratibu huo, Mwampombe alisema, hutumia hadhira hususani zinazowahusu vijana kukumbushana kuhusiana na mapambano hayo.
Baraza la Vijana wa Temeke, hufanyika kila mwaka mara moja likiwajumuisha wajumbe wa umoja wa vijana wa vijana kutoka katika kata zote za majimbo ya Temeke na Kigamboni wakilenga kujadiliana masuala mbalimbali yanayohusu mustakabali wa maendeleo yao.

No comments:

Post a Comment