Tuesday 17 September 2013

SEKONDARI YA ILBORU VIPAJI MAALUM YAFUNGWA KWA MUDA USIOJULIKANA KWA HOFU YA KUCHOMWA MOTO...


 SHULE ya Sekondari ya Ilboru, jijini Arusha imefungwa kwa muda usiojulikana kuanzia leo baada ya kuwepo hofu ya kuchomwa moto.


Uchunguzi wa madai ya shule hiyo kuchomwa moto, unaendelea kufanywa huku ikielezwa kwamba wanafunzi wanne wanahojiwa na polisi wilayani Arumeru wasaidie kubaini ukweli juu ya madai hayo.


Wanafunzi wengine 10 inadaiwa wamepewa barua za kusimamishwa shule kwa siku kadhaa wakihusishwa na suala hilo.


Tangazo la kufunga shule hiyo lilitolewa ghafla leo asubuhi na Mkuu wa Shule, Julius Shila baada ya kushauriana na bodi yake, huku polisi wa kawaida wakifanya doria kudhibiti vurugu zozote ambazo zingeweza kutokea.


Ingawa Mkuu wa Shule, Shila hakutaka kuzungumzia suala hilo, Kaimu Ofisa Elimu wa Mkoa, Sifael Mollel, alisema uchunguzi wa madai hayo unaendelea katika kipindi hiki ambacho wanafunzi wamepewa likizo.


Alisema kuwepo kwa hofu hiyo na wasiwasi wa kuzuka vurugu ndiko kulikosababisha shule ifungwe kwa muda licha ya kwamba walikuwa hawajamaliza mitihani.


“Uongozi umeamua wanafunzi warudishwe nyumbani kutokana na hofu ya kuchomwa moto shule, wanafunzi walikuwa wakifanya mitihani kabla ya kuanza likizo fupi lakini uwepo tishio hilo na kuzuka kwa vurugu, ilionekana ni vema ikafungwa,” amesema.


Alisema kwa kawaida likizo fupi ni ya siku 10 lakini kwa tukio hili wanafunzi hao wamepewa maelekezo ya kwenda kuonana na wakuu wa wilaya zao kwa udahili kabla ya kurejea tena shuleni.


Akizungumzia vitisho vya moto, alisema wanafunzi hao waliwasilisha barua ofisini kwake wakitoa madai kuwa baadhi ya walimu walikuwa wanataka kuchoma moto shule hiyo.


Alisema polisi walienda kufanya uchunguzi Ijumaa ambapo walinusa harufu ya petroli iliyokuwa imemwagwa jirani na bweni.


Hata hivyo Kaimu Ofisa Elimu huyo hakutawataja wanafunzi ambao wanahojiwa na polisi wala wanafunzi 10 ambao wamesimamishwa kwa siku 21.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Liberatus Sabas, alikiri polisi kuwepo shuleni hapo wakati tangazo la kufungwa shule likitolewa akasema hiyo ilikuwa ni kwa sababu ya kuimarisha usalama.


Kwa mujibu wa tangazo hilo, wanafunzi wote watatakiwa kurejea shuleni hapo baada ya kudahiliwa na wakuu wa wilaya zao.


No comments:

Post a Comment