Tuesday 17 September 2013

MWALIMU ATIWA MBARONI KWA KOSA LA KUWABAKA WANAFUZI WAKE WAWILI NDANI YA SIKU MOJA...!!!


  MWALIMU wa Shule ya Sekondari Mwembeni mkoani Mara, amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya, akikabiliwa na mashitaka mawili ya kuwabaka wanafunzi kwa nyakati tofauti.

Andrew Shadrack (26) ambaye aliwahi kufundisha masomo ya Kingereza na dini katika Shule ya Sekondari ya Montfort wilayani Mbarali mkoani Mbeya alifikishwa mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Kamago Minja.
Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Luchagula Mazoya alidai mwalimu huyo alitenda makosa hayo Septemba 13 mwaka huu usiku.
Katika shitaka la kwanza, Mazoya alidai saa 3:30 usiku wa tarehe hiyo, Mwalimu Shadrack alimbaka kwa nguvu mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Montfort mwenye umri wa miaka 17, aliyekuwa akijisomea baada ya kumwita na kumpeleka gizani.
Alidai katika shitaka lingine, siku hiyo Septemba 13 saa 4:00 ikiwa ni nusu saa kupita baada ya tukio la kwanza, Mwalimu Shadrack alimbaka mwanafunzi mwingine wa kidato cha nne shuleni hapo aliye na umri wa miaka 18, aliyemwita kutoka katika bweni alimokuwa amelala.
Alidai mbinu iliyotumiwa na mshitakiwa kwa wanafunzi hao wote, licha ya kutumia nguvu, alikuwa akiwaahidi mambo mbalimbali, ikiwemo kuwasaidia kimasomo, akiwaeleza kuwa anataraji kurudi shuleni hapo na kushika wadhifa wa ukuu wa shule.
Kutokana na kile kilichodaiwa ni uzito wa mashitaka husika, upande wa walalamikaji uliiomba Mahakama, kutoruhusu dhamana kwa mshitakiwa.
Hakimu Minja alikubaliana na maombi hayo na kufunga dhamana, hivyo mwalimu huyo ataendelea kukaa rumande hadi Septemba 18 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment